Mwaka 2012 ndio huoo umetokomea, ni
vizuri kuangalia yaliyopita ili kujitayarisha na yajayo. Muziki wa nchi yetu
ulitawaliwa na muziki wa Bongoflava, Taarab, muziki wa bendi, matarumbeta,
muziki wa Enjili, na muziki wa kiasili. Si siri kuwa muziki wa Bongoflava ndio
uliokuwa ukitawala katika vyombo vya habari na sehemu nyingi za maonyesho
ukifuatiliwa na muziki wa Taarab na muziki wa enjili. Katika muziki wote huu jambo lililokuwa wazi ni kuwa waimbaji
ndio waliokuwa wakipewa kipaumbele katika tasnia hii. Waimbaji katika aina zote za muziki uliotajwa hapo juu ndio
waliotajwa na kupewa sifa kwa ubora wa muziki. Kumekuweko na mashindano kadhaa
ambayo yote yamejikita katika kutafuta vipawa vya waimbaji japo mara nyingi
yamejitambulisha kama mashindano ya kusaka vipaji mbalimbali. Hakuna ubishi
muziki wa dansi na muziki wa asili ndio muziki uliopewa muda mchache sana
katika vyombo vya habari. Na hata katika muziki huo, bendi ambazo zimejikita
kufuata mipigo ya Kikongo vilipewa nafasi zaidi ya bendi ambazo zimejichagulia
njia nyingine za muziki wao.
Kuna sababu kadhaa ambazo zimefanya
muziki wa bongoflava kuchukua nafasi zaidi katika vyombo vya habari, la kwanza
ni uwingi wa kazi za bongoflava zinazorekodiwa. Karibu kila mji una studio ya
aina moja au nyingine, na katika studio hizo kazi nyingi zaidi zinazorekodiwa
ni aina hiyo ya muziki, hivyo kutokana na uwingi wa kazi hizo ni wazi kabisa
ndizo ambazo zitaendelea kutawala anga la vyombo vya habari, na pia ni kutokana
na mfumo wa vyombo vyetu vyote kujikita katika mfumo wa aina fulani tu za
muziki.
Kwa mtizamo wangu heka heka za muziki
wa Enjili zilipungua 2012. Yale matamasha makubwa ya muziki huo yalipungua
sana, na hata nyimbo za kushtua jamii hazikuwa nyingi kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Muziki wa Taarab haujaleta mabadiliko
kimuziki, mengi yaliyofanywa katika 2012 ni marudio tu ya ubunifu uliofanyika
nyuma. Kama vile uanzishwaji wa kucheza show katika taarab, upigaji wa gitaa na
kuliachia pekee yake kama ilivyokuwa kwa bendi kuachia gitaa la rhythm miaka
kabla ya tisini na zile video za kucheza mbele za viwanja vya hoteli.
Kumekuweko tu ubunifu wa misemo na mipasho, jambo tena ambalo limesababisha
kuenziwa zaidi kwa waimbaji tu katika fani hiyo pia.
Bendi ziko katika wakati mgumu, wakati
wanamuziki wengi wa bendi wakilalamika kuwa muziki wa bendi haupigwi,
kumekuweko na jitihada ndogo za bendi kurekodi nyimbo mpya, maelezo mengi
yamekuwa ni kuhadithia enzi ambapo muziki wa bendi ulitawala na kuona kama hiyo
ni sababu tosha ya muziki huo kurushwa hewani. Bendi chache zilizorekodi
hazijaja na nyimbo zilizoweza
kuteka umma wa wa Tanzania na hivyo kusababisha muziki huu kukosekana katika
anga za muziki. Matangazo mengi ya muziki wa dansi yamekuwa ni kutangaza rap
mpya au kupatikana kwa msanii mpya, lakini kiujumla hakujakuwa na kitu kipya
katika muziki wa bendi.
Muziki asili pia umekosekana kwenye
vyombo vya habari kwa kuwa si vikundi vingi vya muziki huu vyenye uwezo wa
kulipia gharama za studio ambao muziki huu unastahili kurekodiwa. Studio nyingi
zimejengwa kwa ajili ya muziki wa aina ya Bongoflava tu, zile studio za kuweza
kuruhusu kundi la muziki wa asili kurekodi gharama yake huwa ni kubwa
sana.
Kundi la Makirikiri lilitakiwa kuwa
elimu tosha kwa wasanii wa muziki wa Kiasili, kuwa na muziki huo ukifuata
taratibu nzuri ya kurekodiwa unauza vizuri sana, bahati mbaya kuna vikundi sasa
vimeacha muziki na ngoma zao, vinaiga uchezaji wa Makirikiri.
Pengine watu watasema nimesahau muziki
wa kwaya, sijausahau, kwa kweli muziki huu umebaki hasa kwenye muziki wa Enjili. Hapo zamani ulikuwa ukitumika
sana kwenye siasa na kampeni , lakini kwa mwaka 2012 hali imekuwa mbaya kwa
muziki huu.
Pamoja na kuwa wengine wangeweza kusema
tunasonga mbele katika muziki, kwangu mimi naona tunarudi nyuma kitaaluma.
Tasnia inaingiza pesa nyingi zaidi, na hata kuna wasanii walioingiza pesa
nyingi sana, lakini kwangu hilo si
kipimo cha maendeleo katika tasnia hii.
Kama nilivyoanza kusema washika
maikrofon wamekuwa ndio alama ya muziki wa Tanzania. Muziki ni zaidi ya kuimba.
Katika kuimba sauti nzuri ya muimbaji ni muhimu, na ninashukuru kwa hilo tunao
waimbaji wazuri wengi sana, lakini
ule muziki unaomsindikiza muimbaji ni muhimu sana kwani ule hauna mipaka
wala lugha, na ndio unaoweza kutufungulia mlango wa soko la kimataifa. Wengi
tunapenda sana muziki wa kutoka Kongo, Nigeria, South Africa, pamoja na kuwa
hatujui hata moja wanaloliongelea tunaupenda muziki huo kutokana na mpangilio
wa vyombo vyao. Kutokujali wapigaji katika mfumo wa nchi yetu ndio unatupelekea
kuwa watu wa ‘copy and paste’ wa upigaji wa muziki wa nchi nyingine.
Ukiorodhesha nyimbo zote zilizotikisa nchi hii kwa mwaka 2012 utagundua
asilimia kubwa ya muziki uliotumika ulikuwa ni wa kunakili kutoka muziki wa
nchi nyingine, Nigeria, Congo na Afrika Kusini ndio wamekuwa waalimu wetu
wakuu. Ushauri kwa maproducer wa Bongoflava, kuangalia pia muziki wetu wa asili
humu ndani ya nchi ili tuje tumalize 2013 na kitu chetu ambacho Wanaigeria,
Wakongo nao pia waige toka kwetu. Inawezekana sana maana wimbo wa Weekend wa
Afro70 uliwahi kuweko katika kumi
bora 1972, Nigeria.
Muziki wa Enjili pamoja na kuwa ndio
unaotegemewa kutufundisha maadili, ulikuwa na kasoro moja kubwa nayo ni kukosa
maadili kwa kucopy na kupaste. Nyimbo nyingi zilizokuwa maarufu na kuteka hisia
za maelfu ya watu zilikuwa ni kuiga moja kwamoja kutoka Afrika ya kusini.
Najiuliza je ndio kilichopunguza moto wa muziki huu 2012? Kulikuwa hakuna za
kukopi? Wanamuziki wa Enjili kama ilivyo kwa ushauri kuhusu Bongoflava, ni muda
wa kurudi nyuma na kutumia raslimali ya utamaduni iliyoko kuleta mabadiliko na
kukuza soko la muziki huo.
Tasnia ya muuziki wa Tanzania katika
tafiti moja wapo umeitwa ‘the radio-driven contemporary music industry’. Kwa
maneno rahisi, tasnia ambayo imekuwa inaendeshwa na radio. Radio zimekuwa na
uwezo wa kumpandisha na kumshusha mwanamuziki, kumtafutia soko, kumzibia soko
na kadhalika. Hali hii ikisindikizwa na rushwa ambayo imetapakaa katika jamii
yetu, unapata picha kuwa kungeweza kukawa na sura bora au tofauti ya muziki
hali isingekuwa ilivyo. Kuna ripoti za watu kutoa hongo nyimbo za wenzao
zisipigwe, hongo ili nyimbo zipigwe, visasi vya kuzuia nyimbo zisipigwe na
kadhalika. Na katika jamii ambayo imekuwa na kawaida ya kutegemea vyombo vya
habari kujua muziki gani mpya na mzuri, uwanja huu si uwanja ulio tambarare
hata kidogo. Bahati mbaya inaonekana wenye vyombo hivi wako mbali na ukweli
unaoendelea katika vyombo vyao au kwa kutokujua au kupuuza. Janga hili
limevikumba hata vyombo ambavyo vinaendeshwa na taasisi za dini. Wanamuziki wa
muziki wa Enjili nao pia wanalia kudaiwa rushwa na watangazaji wa radio za
Enjili!. Nakumbuka siku niliyopata
nafasi kuongea na kiongozi mmoja wa dini ambaye Kanisa lake linaendesha kituo
cha radio, nilipata mshangao baada mkuu huyo, kuanza kutetea watangazaji wake
badala ya kuamua kufanya uchunguzi wa tuhuma.
Umefika muda wa radio kuanza kujigawa
kimuziki. Ni kichekesho mji kuwa na vituo vya radio 30 halafu vyote vinapiga
aina hiyohiyo ya muziki, wakati kuna aina mbalimbali za watu. Ajabu ni kuwa
wenye radio wanajua kuwa katika nchi nyingine unaweza kukuta radio iliyoamua
kupiga aina fulani tu ya muziki, Jazz Radio, Country music Radio, Classic Music
Radio, lakini hilo limekuwa gumu kwao kutekeleza hapa. Kuwe na utofauti,
Wasikilizaji tuko wa aina tofauti.
Vyombo vya habari viijitahidi kupata
wataalamu husika wa aina tofauti za muziki, muziki unaviingizia vyombo hivyo
mabilioni ya fedha, vyombo vya habari
viupe heshima yake. Bila muziki hakuna radio.
Magazeti yamekuwa mstari wa mbele
katika kutangaza aina mbalimbali za wasanii na sanaa. Pamoja na hongera kwa
kazi nzuri lakini bado kuna nafasi kubwa ipo tupu, hakuna wataalamu wa uandishi
wa habari za muziki. Hivyo habari nyingi za muziki zinaandikwa na waandishi
kama wapenzi wa muziki na si wataalam wa uandishi wa muziki, jambo ambalo liko
tofauti na uandishi wa michezo kwa mfano soka. Unaweza ukasoma habari ya soka
ambapo mwandish atakueleza nafasi za wachezaji, kama ni faulo, ni nini
kilisababisha, na kama ni goli lilikuwa ni la kichwa au kona au penalty, hili
haliko katika muziki. Utaambiwa tu
bendi ilipagawisha, au msanii fulani ateka nyoyo za wapenzi, na maelezo
ya juu juu kama yale, kunahitajika kuanzishwa mafunzo ya elimu ya uandishi wa
kazi za sanaa. Hili litapunguza hata vurugu kama zilizotawala mwaka huu
ya wapiga picha kufikia hata kulala chini ili tu wapate picha ya nguo za ndani
za msanii na hayo ndio kuwa maelezo makuu ya onyesho zima la muziki.
Ikiwa kulikuwa na mchango wa serikali
katika muziki, basi ulikuwa mdogo au ulikuwa ni kwa shughuli maalumu lakini si
kwa kutengeneza mazingira ya kuwezesha unafuu kwa wanamuziki kwa ujumla. Idara
ya Utamaduni imeendelea kupata bajeti ndogo ambayo imefanya Baraza La Sanaa La
Taifa kuendelea kubaki Dar es Salaam tu, likibangaiza kuweko kwa kutegemea
kutoa vibali mbalimbali kwa wasanii, na nguvu zake kuonekana Dar es Salaam tu.
Na kwa kuwa hakuna Maafisa Utamaduni Mkoa, na Maafisa Utamaduni Wilaya na
Manispaa wako chini ya serikali za mitaa hivyo kuwa wizara tofauti na Waziri wa
Utamaduni, nguvu za serikali katika utamaduni ni 0. COSOTA chombo ambacho
shughuli yake ilikuwa ni kulinda hakimiliki za wasanii na ambacho kilikuwa
chini ya wasanii, kwa kinyemela kabisa kimerudishwa katika mikono ya serikali,
lakini bado kinakusanya mirabaha 'kwa niaba ya wasanii' huku kukiwa na bodi
isiyo na uwakilishi wa wasanii kuanzia 2007. Swali utakusanyaje pesa kwa iaba
yangu lakini huniruhusu kujua ni kiasi gani umekusanya, unazitumiaje na
ukiulizwa unakuwa mkali!!!!!!? Kuna wasanii wamekuwa wakidai kurudishiwa
COSOTA, ushauri wangu wasanii wakae wajipange na kuelewa vizuri sheria ya
Hakimiliki kabla ya kujitwishwa zigo hilo la miba.
Katika miezi 6 ya mwisho ya 2012
kumejitokeza spidi kali ya Mamlaka ya Ukusanyaji wa Mapato kutengeneza
mazingira ya kukusanya mapato kutokana na mauzo ya kazi za muziki na filamu.
Kimsingi kulipa kodi ni wajibu wa kila mwananchi na wasanii ni wananchi pia,
lakini taratibu zake ndio zinanipa utata, hasa pale ambapo kwa muda mrefu
imekuwa ikitangazwa kuwa njia hii itasaidia wasanii kwa kupunguza kuibiwa. Sentensi hii inaonyesha wazi
anaeiongelea aidha hajui mfumo wa biashara ya kazi muziki, au kwa makusudi
anapotosha ili kuficha kitu. Wasanii wengi huwa wamekwishalipwa kwa kazi ambazo
zimesambaa na ziko barabarani zinaibiwa, wanaoibiwa ni wasambazaji. Hivyo
kulinda kazi hizo unamlinda msambazaji si msanii. Pia kuanza kukusanya kodi kwa
kazi hizi kumepewa jina ‘kurasmishwa
kwa kazi ya usanii’, kuna mabilioni wasanii wanatakiwa walipwe na
watumiaji wa kazi za sanaa, kama radio na TV, mapromota, waajiri na
kadhalika hakuna anaeliongelea hilo wala hakuna anaetamka takwimu hizo.
Kuna kazi ya kurudisha mitaala ya masomo ya sanaa mashuleni, kurudisha vyuo vya
walimu wa sanaa, kurudisha maafisa utamaduni kuwa chini ya Wizara ya Utamaduni
kuwawezesha kufanya kazi zao kadri ya sera ya Utamaduni, na mengine mengi ya
aina hiyo ndio ningeona kurasimisha kazi za sanaa, lakini kukusanya kodi tu kwa
kazi ambazo hata hivyo mikataba yake mingi inautata na kuita urasimishaji si
sahihi.
Katika nchi nyingi critics au watu
ninaoweza kuwaita kiswahili wakosoaji, huwa ni muhimu katika maendeleo ya
sanaa, watu hawa hupata heshima kutokana na kuweza kuangalia mapungufu katika
kazi za sanaa na kuyasema, jambo ambalo hupelekea wasanii kujirekibisha na
kutengeneza kazi bora zaidi. Hapa kwetu kutoa ushauri ni kutafuta matusi, toka
kwa wasanii wenye kazi husika, vyombo vya habari na hata sehemu ya jamii, umefika
muda wahusika kuchukua uchambuzi kama changa moto za kuboresha kazi.
Niliyoyataja hapa yote yako wazi
ninachotegemea ni kuona 2013, hatua zinaanza kupigwa kurekibisha, ili
wanamuziki wa nchi hii nao wapate nafasi sawa na wengine wa nchi nyingine.
John Kitime
31.12.2012
Sinza, Dar es Salaam