Tuesday, January 22, 2013

KAZI ZA COSOTA


47. The functions of the society shall be
a) to promote and protect the interests of authors, performers, translators, producers of sound recordings, broadcasters,
publishers, and, in particular, to collect and distribute any royalties or
other remuneration accorded to them in respect of their rights provided for in this Act; (Copyright Act No 7 ya 1999)
(b) to maintain registers of works, productions and associations of authors, performers, translators, producers of sound
recordings, broadcasters and publishers;
(c) to search for, identify and publicize the rights of owners and
give evidence of the ownership of these where there is a dispute or an infringement;
(d) to print, publish, issue or circulate any information,
report, periodical, books, pamphlet, leaflet or any other material relating to copyright and rights of performers, producers of sound recordings and broadcasters. to advise the Minister on all matters under this Act.

Monday, December 31, 2012

JICHO LANGU KATIKA MUZIKI 2012


Mwaka 2012 ndio huoo umetokomea, ni vizuri kuangalia yaliyopita ili kujitayarisha na yajayo. Muziki wa nchi yetu ulitawaliwa na muziki wa Bongoflava, Taarab, muziki wa bendi, matarumbeta, muziki wa Enjili, na muziki wa kiasili. Si siri kuwa muziki wa Bongoflava ndio uliokuwa ukitawala katika vyombo vya habari na sehemu nyingi za maonyesho ukifuatiliwa na muziki wa Taarab na muziki wa enjili.  Katika muziki wote huu jambo lililokuwa wazi ni kuwa waimbaji ndio waliokuwa wakipewa kipaumbele katika tasnia hii.  Waimbaji katika aina zote za muziki uliotajwa hapo juu ndio waliotajwa na kupewa sifa kwa ubora wa muziki. Kumekuweko na mashindano kadhaa ambayo yote yamejikita katika kutafuta vipawa vya waimbaji japo mara nyingi yamejitambulisha kama mashindano ya kusaka vipaji mbalimbali. Hakuna ubishi muziki wa dansi na muziki wa asili ndio muziki uliopewa muda mchache sana katika vyombo vya habari. Na hata katika muziki huo, bendi ambazo zimejikita kufuata mipigo ya Kikongo vilipewa nafasi zaidi ya bendi ambazo zimejichagulia njia nyingine za muziki wao.
Kuna sababu kadhaa ambazo zimefanya muziki wa bongoflava kuchukua nafasi zaidi katika vyombo vya habari, la kwanza ni uwingi wa kazi za bongoflava zinazorekodiwa. Karibu kila mji una studio ya aina moja au nyingine, na katika studio hizo kazi nyingi zaidi zinazorekodiwa ni aina hiyo ya muziki, hivyo kutokana na uwingi wa kazi hizo ni wazi kabisa ndizo ambazo zitaendelea kutawala anga la vyombo vya habari, na pia ni kutokana na mfumo wa vyombo vyetu vyote kujikita katika mfumo wa aina fulani tu za muziki.
Kwa mtizamo wangu heka heka za muziki wa Enjili zilipungua 2012. Yale matamasha makubwa ya muziki huo yalipungua sana, na hata nyimbo za kushtua jamii hazikuwa nyingi  kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Muziki wa Taarab haujaleta mabadiliko kimuziki, mengi yaliyofanywa katika 2012 ni marudio tu ya ubunifu uliofanyika nyuma. Kama vile uanzishwaji wa kucheza show katika taarab, upigaji wa gitaa na kuliachia pekee yake kama ilivyokuwa kwa bendi kuachia gitaa la rhythm miaka kabla ya tisini na zile video za kucheza mbele za viwanja vya hoteli. Kumekuweko tu ubunifu wa misemo na mipasho, jambo tena ambalo limesababisha kuenziwa zaidi kwa waimbaji tu katika fani hiyo pia.
Bendi ziko katika wakati mgumu, wakati wanamuziki wengi wa bendi wakilalamika kuwa muziki wa bendi haupigwi, kumekuweko na jitihada ndogo za bendi kurekodi nyimbo mpya, maelezo mengi yamekuwa ni kuhadithia enzi ambapo muziki wa bendi ulitawala na kuona kama hiyo ni sababu tosha ya muziki huo kurushwa hewani. Bendi chache zilizorekodi hazijaja na  nyimbo zilizoweza kuteka umma wa wa Tanzania na hivyo kusababisha muziki huu kukosekana katika anga za muziki. Matangazo mengi ya muziki wa dansi yamekuwa ni kutangaza rap mpya au kupatikana kwa msanii mpya, lakini kiujumla hakujakuwa na kitu kipya katika muziki wa bendi.
Muziki asili pia umekosekana kwenye vyombo vya habari kwa kuwa si vikundi vingi vya muziki huu vyenye uwezo wa kulipia gharama za studio ambao muziki huu unastahili kurekodiwa. Studio nyingi zimejengwa kwa ajili ya muziki wa aina ya Bongoflava tu, zile studio za kuweza kuruhusu kundi la muziki wa asili kurekodi gharama yake huwa ni kubwa sana. 
Kundi la Makirikiri lilitakiwa kuwa elimu tosha kwa wasanii wa muziki wa Kiasili, kuwa na muziki huo ukifuata taratibu nzuri ya kurekodiwa unauza vizuri sana, bahati mbaya kuna vikundi sasa vimeacha muziki na ngoma zao, vinaiga uchezaji wa  Makirikiri.
Pengine watu watasema nimesahau muziki wa kwaya, sijausahau, kwa kweli muziki huu umebaki  hasa kwenye muziki wa Enjili. Hapo zamani ulikuwa ukitumika sana kwenye siasa na kampeni , lakini kwa mwaka 2012 hali imekuwa mbaya kwa muziki huu.
Pamoja na kuwa wengine wangeweza kusema tunasonga mbele katika muziki, kwangu mimi naona tunarudi nyuma kitaaluma. Tasnia inaingiza pesa nyingi zaidi, na hata kuna wasanii walioingiza pesa nyingi sana, lakini  kwangu hilo si kipimo cha maendeleo katika tasnia hii.
Kama nilivyoanza kusema washika maikrofon wamekuwa ndio alama ya muziki wa Tanzania. Muziki ni zaidi ya kuimba. Katika kuimba sauti nzuri ya muimbaji ni muhimu, na ninashukuru kwa hilo tunao waimbaji wazuri wengi sana, lakini  ule muziki unaomsindikiza muimbaji ni muhimu sana kwani ule hauna mipaka wala lugha, na ndio unaoweza kutufungulia mlango wa soko la kimataifa. Wengi tunapenda sana muziki wa kutoka Kongo, Nigeria, South Africa, pamoja na kuwa hatujui hata moja wanaloliongelea tunaupenda muziki huo kutokana na mpangilio wa vyombo vyao. Kutokujali wapigaji katika mfumo wa nchi yetu ndio unatupelekea kuwa watu wa ‘copy and paste’ wa upigaji wa muziki wa nchi nyingine. Ukiorodhesha nyimbo zote zilizotikisa nchi hii kwa mwaka 2012 utagundua asilimia kubwa ya muziki uliotumika ulikuwa ni wa kunakili kutoka muziki wa nchi nyingine, Nigeria, Congo na Afrika Kusini ndio wamekuwa waalimu wetu wakuu. Ushauri kwa maproducer wa Bongoflava, kuangalia pia muziki wetu wa asili humu ndani ya nchi ili tuje tumalize 2013 na kitu chetu ambacho Wanaigeria, Wakongo nao pia waige toka kwetu. Inawezekana sana maana wimbo wa Weekend wa Afro70 uliwahi kuweko katika  kumi bora 1972, Nigeria.
Muziki wa Enjili pamoja na kuwa ndio unaotegemewa kutufundisha maadili, ulikuwa na kasoro moja kubwa nayo ni kukosa maadili kwa kucopy na kupaste. Nyimbo nyingi zilizokuwa maarufu na kuteka hisia za maelfu ya watu zilikuwa ni kuiga moja kwamoja kutoka Afrika ya kusini. Najiuliza je ndio kilichopunguza moto wa muziki huu 2012? Kulikuwa hakuna za kukopi? Wanamuziki wa Enjili kama ilivyo kwa ushauri kuhusu Bongoflava, ni muda wa kurudi nyuma na kutumia raslimali ya utamaduni iliyoko kuleta mabadiliko na kukuza soko la muziki huo.
Tasnia ya muuziki wa Tanzania katika tafiti moja wapo umeitwa ‘the radio-driven contemporary music industry’. Kwa maneno rahisi, tasnia ambayo imekuwa inaendeshwa na radio. Radio zimekuwa na uwezo wa kumpandisha na kumshusha mwanamuziki, kumtafutia soko, kumzibia soko na kadhalika. Hali hii ikisindikizwa na rushwa ambayo imetapakaa katika jamii yetu, unapata picha kuwa kungeweza kukawa na sura bora au tofauti ya muziki hali isingekuwa ilivyo. Kuna ripoti za watu kutoa hongo nyimbo za wenzao zisipigwe, hongo ili nyimbo zipigwe, visasi vya kuzuia nyimbo zisipigwe na kadhalika. Na katika jamii ambayo imekuwa na kawaida ya kutegemea vyombo vya habari kujua muziki gani mpya na mzuri, uwanja huu si uwanja ulio tambarare hata kidogo. Bahati mbaya inaonekana wenye vyombo hivi wako mbali na ukweli unaoendelea katika vyombo vyao au kwa kutokujua au kupuuza. Janga hili limevikumba hata vyombo ambavyo vinaendeshwa na taasisi za dini. Wanamuziki wa muziki wa Enjili nao pia wanalia kudaiwa rushwa na watangazaji wa radio za Enjili!.  Nakumbuka siku niliyopata nafasi kuongea na kiongozi mmoja wa dini ambaye Kanisa lake linaendesha kituo cha radio, nilipata mshangao baada mkuu huyo, kuanza kutetea watangazaji wake badala ya kuamua kufanya uchunguzi wa tuhuma.
Umefika muda wa radio kuanza kujigawa kimuziki. Ni kichekesho mji kuwa na vituo vya radio 30 halafu vyote vinapiga aina hiyohiyo ya muziki, wakati kuna aina mbalimbali za watu. Ajabu ni kuwa wenye radio wanajua kuwa katika nchi nyingine unaweza kukuta radio iliyoamua kupiga aina fulani tu ya muziki, Jazz Radio, Country music Radio, Classic Music Radio, lakini hilo limekuwa gumu kwao kutekeleza hapa. Kuwe na utofauti, Wasikilizaji tuko wa aina tofauti.
Vyombo vya habari viijitahidi kupata wataalamu husika wa aina tofauti za muziki, muziki unaviingizia vyombo hivyo mabilioni ya fedha, vyombo vya habari  viupe heshima yake. Bila muziki hakuna radio.
Magazeti yamekuwa mstari wa mbele katika kutangaza aina mbalimbali za wasanii na sanaa. Pamoja na hongera kwa kazi nzuri lakini bado kuna nafasi kubwa ipo tupu, hakuna wataalamu wa uandishi wa habari za muziki. Hivyo habari nyingi za muziki zinaandikwa na waandishi kama wapenzi wa muziki na si wataalam wa uandishi wa muziki, jambo ambalo liko tofauti na uandishi wa michezo kwa mfano soka. Unaweza ukasoma habari ya soka ambapo mwandish atakueleza nafasi za wachezaji, kama ni faulo, ni nini kilisababisha, na kama ni goli lilikuwa ni la kichwa au kona au penalty, hili haliko katika muziki. Utaambiwa tu  bendi ilipagawisha, au msanii fulani ateka nyoyo za wapenzi, na maelezo ya juu juu kama yale, kunahitajika kuanzishwa mafunzo ya elimu ya uandishi wa kazi za sanaa. Hili litapunguza hata vurugu kama zilizotawala  mwaka huu ya wapiga picha kufikia hata kulala chini ili tu wapate picha ya nguo za ndani za msanii na hayo ndio kuwa maelezo makuu ya onyesho zima la  muziki.
Ikiwa kulikuwa na mchango wa serikali katika muziki, basi ulikuwa mdogo au ulikuwa ni kwa shughuli maalumu lakini si kwa kutengeneza mazingira ya kuwezesha unafuu kwa wanamuziki kwa ujumla. Idara ya Utamaduni imeendelea kupata bajeti ndogo ambayo imefanya Baraza La Sanaa La Taifa kuendelea kubaki Dar es Salaam tu, likibangaiza kuweko kwa kutegemea kutoa vibali mbalimbali kwa wasanii, na nguvu zake kuonekana Dar es Salaam tu. Na kwa kuwa hakuna Maafisa Utamaduni Mkoa, na Maafisa Utamaduni Wilaya na Manispaa wako chini ya serikali za mitaa hivyo kuwa wizara tofauti na Waziri wa Utamaduni, nguvu za serikali katika utamaduni ni 0. COSOTA chombo ambacho shughuli yake ilikuwa ni kulinda hakimiliki za wasanii na ambacho kilikuwa chini ya wasanii, kwa kinyemela kabisa kimerudishwa katika mikono ya serikali, lakini bado kinakusanya mirabaha 'kwa niaba ya wasanii' huku kukiwa na bodi isiyo na uwakilishi wa wasanii kuanzia 2007. Swali utakusanyaje pesa kwa iaba yangu lakini huniruhusu kujua ni kiasi gani umekusanya, unazitumiaje na ukiulizwa unakuwa mkali!!!!!!? Kuna wasanii wamekuwa wakidai kurudishiwa COSOTA, ushauri wangu wasanii wakae wajipange  na kuelewa vizuri sheria ya Hakimiliki kabla ya kujitwishwa zigo hilo la miba.
Katika miezi 6 ya mwisho ya 2012 kumejitokeza spidi kali ya Mamlaka ya Ukusanyaji wa Mapato kutengeneza mazingira ya kukusanya mapato kutokana na mauzo ya kazi za muziki na filamu. Kimsingi kulipa kodi ni wajibu wa kila mwananchi na wasanii ni wananchi pia, lakini taratibu zake ndio zinanipa utata, hasa pale ambapo kwa muda mrefu imekuwa ikitangazwa kuwa njia hii itasaidia wasanii kwa kupunguza kuibiwa.  Sentensi hii inaonyesha wazi anaeiongelea aidha hajui mfumo wa biashara ya kazi muziki, au kwa makusudi anapotosha ili kuficha kitu. Wasanii wengi huwa wamekwishalipwa kwa kazi ambazo zimesambaa na ziko barabarani zinaibiwa, wanaoibiwa ni wasambazaji. Hivyo kulinda kazi hizo unamlinda msambazaji si msanii. Pia kuanza kukusanya kodi kwa kazi hizi kumepewa jina ‘kurasmishwa  kwa kazi ya usanii’, kuna mabilioni wasanii wanatakiwa walipwe na watumiaji wa kazi za sanaa, kama radio na TV, mapromota, waajiri na kadhalika  hakuna anaeliongelea hilo wala hakuna anaetamka takwimu hizo. Kuna kazi ya kurudisha mitaala ya masomo ya sanaa mashuleni, kurudisha vyuo vya walimu wa sanaa, kurudisha maafisa utamaduni kuwa chini ya Wizara ya Utamaduni kuwawezesha kufanya kazi zao kadri ya sera ya Utamaduni, na mengine mengi ya aina hiyo ndio ningeona kurasimisha kazi za sanaa, lakini kukusanya kodi tu kwa kazi ambazo hata hivyo mikataba yake mingi inautata na kuita urasimishaji si sahihi. 
Katika nchi nyingi critics au watu ninaoweza kuwaita kiswahili wakosoaji, huwa ni muhimu katika maendeleo ya sanaa, watu hawa hupata heshima kutokana na kuweza kuangalia mapungufu katika kazi za sanaa na kuyasema, jambo ambalo hupelekea wasanii kujirekibisha na kutengeneza kazi bora zaidi. Hapa kwetu kutoa ushauri ni kutafuta matusi, toka kwa wasanii wenye kazi husika, vyombo vya habari na hata sehemu ya jamii, umefika muda wahusika kuchukua uchambuzi kama changa moto za kuboresha kazi.
Niliyoyataja hapa yote yako wazi ninachotegemea ni kuona 2013, hatua zinaanza kupigwa kurekibisha, ili wanamuziki wa nchi hii nao wapate nafasi sawa na wengine wa nchi nyingine.

John Kitime
31.12.2012
Sinza, Dar es Salaam



Tuesday, December 4, 2012

SEMINA YA RUSHWA KATIKA SANAA WILAYA YA KINONDONI

Leo tena nilipata bahati ya kuongoza semina ya wasanii wa Wilaya ya Kinondoni katika mada kuhusu rushwa katika tasnia ya sanaa. Baada ya kuwezesha semina ya namna hii kwa wasanii wa wilaya za Temeke na Ilala, nimeweza kufika katika hali ya mshangao kuhusu ukubwa wa tatizo hili katika tasnia hii.Washiriki waliweza kueleza matukio mengi ya rushwa za aina mbalimbali kati ya wasanii kwa wasanii, na wasanii na wadau wengine kama watangazaji, producers, maafisa wa serikali, maafisa masoko, na wadau mbalimbali tena wenye majina ya kuheshika katika jamii, ni aibu. Kuna haja ya viongozi wa vyombo vya utangazaji, na media nyingine kujishusha na kuja kusikiliza hawa wasanii waliyoyapitia kupitia vyombo vyao. Kwa mfano kuna mtangazaji maarufu aliwahi kuagiza aletewe mbuzi na kiroba cha mchele , ili apige nyimbo za wasanii fulani, mchele kachukua na mbuzi kachukua nyimbo hakupiga, pia rushwa ya 'ma middle men' waliopo ili filamu ziwafikie wasambazaji, rushwa za ngono ili kupata nafasi katika filamu, hadithi ni nyingi, wasanii wakweli kuna haja ya kuungana ili kupigana na janga hili chafu






Tuesday, October 2, 2012

BARAZA LA SANAA LATAMKA MAZITO

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limewaagiza viongozi wa Mashirikisho ya sanaa hapa nchini kufuatilia kwa karibu matukio ya ukiukwaji wa maadili yanayoendelea katika Sanaa hivi sasa na kuchukua hatua kwa wanaobainika kufanya hivyo.  Mbali na BASATA kuwakemea vikali wasanii wanaotumia majukwaa kwa kuidhalilisha Sanaa wao wenyewe na watazamaji pia limeyataka mshirikisho kushirikiana na vyama vyao kuwaita wale wote watakaohusika na uvunjwaji wa maadili ili kuwakanya katika hatua ya kwanza na kama wasipoacha tabia hizo Baraza litawafungia kujishughulisha na kazi ya Sanaa hapa nchini. 
“Shirikisho la Muziki limeagizwa kuangalia tungo za wanamuziki zenye maneno yenye lugha isiyofaa, Shirikisho la Sanaa za Ufundi limeagizwa kuwachukulia hatua wasanii wachoraji na wachongaji wanaotengeneza Sanaa zinazokiuka maadili. Aidha Shirikisho la Sanaa za Maonyesho wameagizwa kufuatilia wasanii wote wanaocheza bila staha majukwaani. Na mwisho Shirikisho la Filamu limeagizwa kuwaita, kuwaonya na kuwachukulia hatua wasanii wote katika fani ya Filamu wanaovaa nusu utupu bila kuzingatia husika katika kazi za Sanaa,” Aidha Baraza limewaagiza wamiliki wa kumbi zote za burudani kuzingatia maadili pale ambapo Sanaa zitakuwepo jukwaani na kwamba baraza halitasita kuufungia ukumbi wowote utakaokiuka agizo hilo. Pia vyombo vya usalama vimeombwa kuhakiki muda wa vibali vya maonyesho na bila kuchelewa kuwachukulia hatua stahiki wasiozingatia muda wa maonyesho. Na  wamiliki wa vyombo vya Habari na Wahariri wamekumbushwa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na wasimamizi wa sanaa kwa kutokurusha wala kutangaza maonyesho ambayo kwa njia yoyote yanachangia mmomonyoko wa maadili ya Taifa letu. Kwa suala hili, Baraza linaziomba mamlaka zinazohusika na usimamizi wa uendeshaji wa vyombo vya habari nchini kuingilia kati na kuvichukulia hatua vyombo vya habari ambavyo kila siku vimekuwa mstari wa mbele kueneza wimbi la mmomonyoko wa maadili hapa nchini na kushusha hadhi ya Tasnia/Sekta ya Sanaa nchini. Sanaa ni kazi na Sanaa ni kioo cha Jamii.

Wednesday, September 19, 2012

Rushwa katika tasnia ya sanaa -1

Nilibahatika kuongoza semina ya wasanii mbalimbali kutoka wilaya ya Ilala, ulikuwa ni mkusanyiko wa wasanii wakiwemo, wasanii wa filamu, ngoma, muziki wa dansi, wachoraji wachongaji na kadhalika. Hii ni  moja ya semina nyingi ambazo zimetayarishwa na Chama cha Sanaa za Maonesho Tanzania(CHASAMATA). Katika semina hii mada ilikuwa Athari za rushwa katika tasnia ya Sanaa. Nilianza kwa kueleza uelewa wangu katika swala hili, ambapo pamoja na mengine nilielezea historia ya  rushwa niliyokuwa naifahamu katika tasnia hii ambayo kwa kweli imeanza miaka mingi sana. Baadhi ya mambo yaliyoleta rushwa katika historia ya sanaa, ni mlolongo wa vibali kabla ya kila onyesho. Wakati wa enzi ya chama kimoja, ilikuwa ni makosa kufanya onyesho bila kibali kutoka kwa afisa utamaduni, hata kikundi kikitaka kutoka nje ya mkoa kilihitaji kuomba kibali cha kutoka nje ya mkoa kutoka kwa afisa utamaduni mkoa ambaye alitoa kibali hicho ambacho kiliwasilishwa kwa afisa utamaduni wa mkoa unaokwenda ambae nae alitoa kibali cha kukuruhusu kuingia mkoa wake na kuwaachia maafisa utamaduni wilaya watoe vibali vya kuruhusu kufanya kazi kwenye wilaya zao, huu ulikuwa uwanja mzuri kwa kuombwa rushwa ili uweze kuruhusiwa kufanya kazi zako. Sehemu nyingine iliyokuwa na rushwa ni redio, ambayo hapo awali ilikuwa moja tu RTD, ambayo pia ilikuwa na studio pekee ya kurekodi muziki kwa muda mrefu. Rushwa ilianza pale ambapo ililazimika kupeleka mashahiri ya tungo za muziki kabla haujarekodiwa, kamati iliyokuwepo wakati huo, iliweza kukataa au kukubali wimbo urekodiwe kwenye studio zake baada ya kusoma mashahiri hayo,bila kulazimika kutoa maelezo kuhusu uamuzi huo, hivyo bendi nyingi zilidaiwa kitu kidogo ili kuhakikisha nyimbo ambazo zimefika kwenye kamati hiyo zote zinapita zilivyo, ngazi nyingine ya rushwa ilikuwa inakuja katika kuwapa motisha watangazaji husika kupiga nyimbo katika vipindi vyao, aina ya rushwa ambayo iko mpaka leo. Watangazaji wamedaiwa kuomba fedha, vocha za simu, rushwa ya ngono, na hata wengine kutaka vikundi kutoka mikoani kuwaletea mchele, mbuzi nakadhalika.
Rushwa nyingine ilikuwa inatolewa kwa viongozi wa serikali katika kupata kibali cha vikundi kutoka nje ya nchi, kwani taratibu zilikuwa wazi kuwa kikundi hakiwezi kutoka nje ya nchi mpaka Mkurugenzi wa Utamaduni atakapopitisha kibali hicho, Mkurugenzi mmoja ametajwa kuwa alikuwa maarufu kwa kulazimisha kipengele cha kuambatana na kikundi kwenye safari za nje, na kama hakukuwa na uwezekano huo pesa ilikuwa lazima itolewe au la hakuna kibali, wasanii wengi walikosa kwenda nje au wengine waliamua kuchukua sheria mkononi na kusafiri kwa njia za panya. Tatizo hili limedhihirika kuwa bado liko baada msani mmoja kutoa mfano wa Afisa wa Wizara ya Utamaduni, kugoma kusoma na kupitisha ripoti moja ambayo ingefungua mlango wa vikundi hata 40 vya ngoma za kiasili kupata nafasi kuzuru Uchina, na kudai msanii atafute shilingi milioni moja kwa ajili ya kikao cha kuchambua ripoti hiyo, ambayo kwa sasa imerudi kwenye makabati, na hakuna wasanii waliopata nafasi ya kutumia nafasi hiyo adimu.
Pia imedhihirika kuwa bado kuna Maafisa Utamaduni wanapenda rushwa kiasi cha kuwezesha vikundi kushinda katika mashindano mbalimbali kwa makubaliano ya kugawana zawadi. Ilitolewa mifano ambapo Afisa mmoja alidai khanga 5 kati ya 20 zilizotolewa kama zawadi kwa kikundi alichokisaidia kushinda na pia alidai kupewa wheelbarrow ambayo kikundi kilishinda katika mashindano mengine.